Mkakati, mpango kazi kuimarisha mianzi wazinduliwa

NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki, amezindua mkakati wa uimarishaji wa miti ya mianzi na kueleza kuwa tafiti zimebaini kuwepo kwa takribani hekta milioni 12.5 zinaweza kuuteshwa miti hiyo nchini ili kuzuia mmomonyoko wa ardhi na kunyonya hewa ukaa.

Amesema utafiti huo unaonesha Tanzania inapoteza eneo la misitu yenye ukubwa wa hekta zaidi la 469,000 kila mwaka, hali ambayo sio nzuri na halikubaliki hivyo juhudi za pamoja zinahitajika.

Kairuki alieleza hayo jana wakati akizindua mkakati wa kitaifa wa mianzi na mpango kazi wa mkakati huo uliofanyika katika Chuo cha Taifa cha Utalii, Dar es salaam.

Alisema miti ya mianzi ina nafasi kubwa katika uhifadhi wa mazingira kwa kufyonza hewa ya ukaa (carbondioxide) kwa zaidi ya mara 40, hivyo  zao hilo ni muhimu katika utunzaji wa mazingira na kupunguza  athari za mabadiliko ya Tabianchi.

WAZIRI Kairuki akiwa na Katibu Mkuu Abbas, Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya bunge ya Ardhi, Maliasili na Utali - Timotheo Mnzava (kulia) na Mwakilishi wa Mkuu wa mkoa wa Dar es salam.

Alieleza kuwa mkakati huo wa mwaka 2023 - 2031, ambao wenye kauli mbiu ‘Tanzania inawekeza katika Mianzi  kwa ajili ya uhimilivu na kuwa na uchumi endelevu’ unalenga kuimarisha uchumi na wananchi kuweza kupata kipato kutokana na manufaa yaliyopo katika mianzi.

Sambamba na hayo Waziri Kairuki alieleza kuwa mianzi inasaidia  kuimarisha katika mifumo ya ikolojia na kuchangia  kutekeleza nia ya nchi ni  kuokoa hekta milioni 5.2 ifikapo mwaka 2030.
“Pamoja na hayo, nchi  itaweza kupata kodi na fedha za kigeni katika kuchangia pato la taifa katika kukuza uchumi hivyo kuandaliwa kwa mkakati huo ni moja ya utekelezaji wa sera ya taifa ya Misitu ya mwaka 1998 na mkakati kwamba utekelezaji wake ni wa miaka 10 yaani kuanzia 2021 – 2031”, alieleza Kairuki.

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki, akikabidhi mkakati wa kitaifa wa mianzi na mpango kazi wake kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Timotheo Mnzava mara baada ya kuuzindua.

Aidha aliongeza kuwa Idara ya Misitu na Nyuki imekasimiwa kuwa dhamana wa sera, sheria, kanuni na miongozo kwa namna ambavyo wanaweza kuratibu vyema kazi, pamoja na kulishukuru Shirika la kimataifa la Mianzi Duniani (INBAR) kwa kuwapa ushauri wa kitaalamu na ufadhili wa kifedha katika uandaaji wa mkakati huo.

Alisema kuhakikisha kila mtanzania anachukua nafasi yake ya kupanda miti na kuendeleza kwa manufaa ya kizazi kijacho na cha sasa, ambapo alitoa wito kwa Chuo cha Viwanda cha Moshi na SIDO kuendeleza kutafuta teknolojia ya kuchakata zao la mianzi kuongeza mnyororo wa thamani ili kuweza kuuza ndani na nje ya nchi.


MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la kimataifa la Mianzi Duniani, Balozi Ally Mchumo, akipokea kitabu cha mkakati wa kitaifa na mpango kazi wa uimarishaji wa miti ya mianzi toka kwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki mara baada ya kuuzindua.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Mianzi Duniani, Balozi Ally Machumo alisema mianzi inasaidia katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuzuia matumizi ya plastiki.

Alieleza kuwa mti huo unaweza kutengenezwa bidhaa mbali mbali vikiwemo vifaa vya matumizi ya nyumbani kama vikombe na vitu vyengine.

“Mwakani kutakuwa na mkutano wa kimataifa wa mianzi wa Afrika nchini Tanzania, hivyo mkakati huu umekuja wakati muafaka katika kukuza zao la mianzi nchini ambapo Tanzania ilikuwa nchi wanachama tokea mwaka 1997 lilipoanza utafiti wake”, alieleza Balozi Machumu.

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki (kulia), akimkabidhi Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Hassan Abbas, mkakati wa kitaifa wa mianzi na mpango kazi wa mkakati huo mara baada ya kuuzindua hafla iliyofanyika katika Chuo cha Taifa cha Utalii, Dar es salaam.

Mapema Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Hassan Abass alisema mianzi inapopandwa katika eneo la makaazi inasaidia kuweka hewa mzuri na kuleta furaha na baraka katika nyumba pamoja.

Akizungumza na wandishi wa habari, Kamishna wa wakala wa misiti nchini (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, alisema mkakati huo utaifanya Tanzania kuwa sehemu ya nchi 50 duniani wanachama wa shirika la kimataifa la mianzzi kutumia miti hiyo kama mmea wa faida.




 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango