Wadau uwindaji kitalii wachangia miradi ya maendeleo

NA MWANDISHI WETU, ARUSHA

UWINDAJI wa kitalii umechangia kiasi cha Dola 2,546,295 za Marekani sawa na Shilingi bilioni 6,606,635,525 ndani ya kipindi cha 2020/2021 na 2022/2023.

Fedha hizo zimetolewa kwenye miradi mbali mbali ya maendeleo na uendelezaji na shughuli za uhifadhi kwenye Maeneo ya Hifadhi za Wanyamapori za Jamii (WMA).

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Dunstan Kitandula, alieleza hayo alipokuwa anafungua warsha ya wadau wa uhifadhi wa mnyama tembo kwenye mifumo ya ikolojia inayovuka mipaka ya nchi jijini Arusha.

Aidha Kitandula alisema kuwa pamoja na mchango mkubwa unaotolewa na uwindaji wa kitalii kwenye mifumo ikolojia inayovuka mipaka ya nchi, ipo haja ya kuchanganua changamoto za matumizi ya wanyamapori hao zinazochangiwa na wanyama hao kupatikana katika mifumo ya ikolojia inayovuka mipaka ya nchi hivyo tembo hutoka nchi moja kwenda nchi nyingine.

Kitandula aliongeza kuwa katika warsha hiyo anategemea kuwa wadau mbalimbali wa uhifadhi watapata fursa ya kujadiliana changamoto hizo, kupeana uzoefu na mwisho watatoka na majibu ya namna bora ya kutatua changamoto zinazotokana na usimamizi wa mnyama tembo kwenye mifumo ikolojia iliyohifadhiwa ambayo inavuka mipaka nchi.

 “Lengo ni kuhakikisha kuwa uwindaji wa tembo unafaidisha jamii lakini pia unachangia katika uhifadhi na uchumi wa Taifa kwa ujumla kupitia maandalizi miongozo na kanuni zitakazowezesha uwindaji wa tembo kwa maendeleo na uhifadhi”, alisema Kitandula.

Vilevile Kitandula kwa niaba ya Waziri wa Maliasili, Angela Kairuki alimpongeza na Raisi wa taasisi ya Conservation Force (CF) John Jackson, kwa juhudi kubwa alizofanya katika kusaidia uhifadhi wa mnyama tembo kupitia uwindaji wa kitalii lakini pia kusaidia Tanzania katika utekelezaji  wa Mkataba wa Kimataifa wa Biashara ya Wanyamapori na mimea iliyo hatarini kutoweka (CITES) na  kupambana biashara haramu ya nyara nchini Marekani.

 


Comments

Popular posts from this blog

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

SMZ yawaita vijana kushiriki kilimo