‘Uchaguzi serikali za mitaa kuzingatia falsafa ya 4R’

NA SAIDA ISSA, DODOMA

IMEELEZWA kuwa uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2024 utazingatia maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan kama ambavyo amekuwa akizungumza katika majukwaa mbali mbali akisisitiza falsafa ya ‘4R’ kwa maana ya maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na kujenga upya.

Hayo yameelezwa jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Festo Dugange, katika kikao cha viongozi wa dini, Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya Kiserikali kujadili rasimu ya kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2024.

Ambapo alisema kuwa uchaguzi huo utazingatia maono hayo ya Mheshmiwa Rais ili kila chama kipate nafasi sawa katika uchaguzi.

"Ndugu washiriki, rasimu za kanuni zilizoandaliwa ni kama ifuatavyo, Rasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Wilaya za Mwaka 2024”, alieleza.

Aliongeza kuwa; “Rasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mtaa na Wajumbe wa Kamati ya Mtaa katika Mamlaka za Miji za Mwaka, 2024, Rasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji za Mwaka, 2024 naRasimu ya Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo za Mwaka, 2024".

Aidha Naibu huyo alisema kuwa lengo la kikao jicho ni kwa ajili ya kupitia rasimu za Kanuni zilizoandaliwa na kutoa maoni yao kwa lengo la kuboresha.

"Ni matumaini yangu kuwa kila mmoja wenu atashiriki kikamilifu na kutumia muda vizuri katika kutoa michango chanya itakayosaidia kuboresha rasimu zilizoandaliwa, Ninapenda kuwashukuru tena kwa ushirikiano wenu na kujitoa kwenu katika kutekeleza shughuli nyingine za maendeleo pamoja na kusaidia jamii,"alisema.

Kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288, uchaguzi wa viongozi wa Serikali za Mitaa hufanyika kila baada ya miaka mitano (5). Kwa kuwa uchaguzi wa mwisho ulifanyika Novemba, 2019, uchaguzi unaofuata utafanyika Novemba, 2024.

Sheria ya Serikali za Mitaa zinampa Mamlaka Waziri Mwenye Dhamana na Serikali za Mitaa kuandaa Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa ajili ya kusimamia uchaguzi husika na Kanuni hizo zitawasilishwa kwenu kwa ajili ya kupata maoni.

Aidha, rasimu ya kanuni mtakazozipitia leo zimezingatia michango na maoni ambayo yamekuwa yakiwasilishwa na wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa kiwemo suala la mgombea kutopita bila kupingwa na Wakurugenzi wa Halmashauri kutosimamia uchaguzi.

"Ndugu washiriki, ninapenda kuwakumbusha kuwa, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limetunga Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ya mwaka 2024 na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024”, alieleza.

“Aidha, Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2024 imefuta sheria ya Taifa ya Uchaguzi ya mwaka 1985 na sheria ya uchaguzi wa Madiwani ya Serikali za Mitaa ya Mwaka 1976", alisema.

Alisema kuwa Marekebisho yaliyofanyika yamezingatia pia maoni ambayo yamekuwa yakitolewa na wadau ikiwemo suala la namna ya kumpata kiongozi pale anapokuwa mkombea mmoja.

"Kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa huandaliwa ili kukidhi matakwa ya kifungu 201A cha Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na kifungu 87A cha Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288 vinavyomtaka Waziri mwenye dhamana na serikali za mitaa kuweka utaratibu wa uchaguzi wa serikali za mitaa kupitia Kanuni, kwa kuzingatia kuwa, vyama vya siasa ni wadau muhimu katika uchaguzi wa cerikali za mitaa, maoni yenu ni muhimu ili kuboresha kanuni zilizoandaliwa", alisema.

"Aidha ushiriki wenu katika maandalizi ya kanuni hizi ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye anataka uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa Mwaka 2024 kuwa huru na haki", alifafanua.

Comments

Popular posts from this blog

Balozi Mpanda ahimiza ubunifu uhifadhi wa mazingira

Vodacom yawapa uhakika wa matibabu mama, watoto wachanga