Takukuru kuongoza vita dhidi ya rushwa SADC

NA MWANDISHI MAALUM, LUSAKA – ZAMBIA

TANZANIA kupitia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), imechukua uongozi wa taasisi za mapambano dhidi ya rushwa katika ukanda wa Kusini mwa Afrika (SADC) ikiwa ni mara ya pili kushika nafasi hiyo.

Katika hotuba yake ya uzinduzi wa  mkutano wa mwaka wa Wakuu wa Mamlaka za Kupambana na Rushwa kwa nchi za SADC, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Francis Chalalima (pichani), ambaye pia ni Mwenyekiti mpya wa kamati ya SADC ya kupambana na rushwa (SACC), ametahadharisha kuhusu hatari ya rushwa kwenye utoaji wa misaada wakati wa dharura.

Chalamila ameeleza kuwa majanga ya dharura kama vile mlipuko wa magonjwa na athari za mabadiliko ya tabia nchi yanaweza kufungua milango ya rushwa katika hatua mbalimbali za ugawaji misaada, ikiwa ni pamoja na udanganyifu, ubadhirifu wa mali, na ukiukwaji wa maadili ya ununuzi.

“Mchakato wa utoaji misaada upo katika hatari kubwa ya kudhibitiwa na rushwa kwa sababu ya haraka na udharura wa hali zinazokuwepo,” amesema Chalamila.

Aliongeza kuwa pia kunaweza kutokea matumizi mabaya ya ngono (sextortion) kama mojawapo ya aina za rushwa zinazoweza kutokea katika kipindi hicho.

Mkutano huo, ukiwa na kaulimbiu isemayo ‘Kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa katika usimamizi wa majanga na huduma za magereza katika ukanda wa SADC’, umeangazia changamoto zinazoikabili nchi wanachama wa SADC katika kukabiliana na rushwa wakati wa kushughulikia dharura.

Hivyo Chalamila alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mikakati imara ya kanda hiyo ili kuhakikisha misaada inawafikia kwa walengwa kwa uadilifu na uwazi.

Aidha Chalamila alimpongeza Mwenyekiti aliyemaliza muda wake, Monica Chipanta Mwansa wa Zambia, kwa uongozi imara katika kutekeleza mpango mkakati wa SADC wa kupambana na rushwa wa mwaka 2023 - 2027, ambao umejikita katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kuongeza uwajibikaji katika usimamizi wa misaada na majanga.

Mkutano huo wa siku tatu, uliofanyika jijini Lusaka, ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka nchi 14 wanachama wa SADC huku Tanzania ikiongoza mapambano hayo kwa mara ya pili baada ya kuwa Mwenyekiti mwaka 2017/2018.

TAKUKURU inatarajiwa kuendelea na juhudi hizi kwa mwaka wa 2024/2025, ikiwa mstari wa mbele katika kuhakikisha ukanda wa SADC unakuwa na mazingira salama na huru dhidi ya vitendo vya rushwa.

 


Comments

Popular posts from this blog

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

SMZ yawaita vijana kushiriki kilimo