Upigaji kura ‘Samia Kalamu Awards’ waanza rasmi

NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

ZOEZI la upigaji kura kwa washiriki wa tuzo Samia Kalamu Awards, limeanza Novemba 11 na litakamilika Novemba 20, mwaka huu.

Tuzo hizo zimeandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Kwa  mujibu  wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari, upigaji kura utahusisha  wananchi kwa asilimia 60 ya  matokeo kwa kuwa ndio walaji wa maudhui na asilimia 40 ya alama za vigezo vya kitaaluma zitatolewa na jopo la majaji.

Watakaopigiwa  kura ni wanahabari na vyombo  vilivyokidhi vigezo  vya kitaaluma  vya uandishi wa habari za maendeleo ambapo makala 1,131 ziliwasilishwa  kutoka  mikoa yote ya Tanzania bara na  Zanzibar kuwania tuzo hizo.

Aidha chambuzi za  kitaaluma 85 zilizokidhi vigezo ambazo zimewekwa tovuti ya Samia Awards na mitandao ya kijamii pia zitapigiwa kura.

Taarifa hiyo imesema tuzo hizo zinalenga kuhamasisha, kukuza na kupanua wigo wa uandisi, utangazaji na uchapishaji wa maudhui ya ndani kupitia vyombo vya habari vya asili na mtandaoni ili kuchochea uandishi wa makala za kina zinazozingatia maendeleo, uwajibikaji, mila na tamaduni.

 “Tunawahimiza wananchi na wadau wa habari kushiriki katika mchakato huu wa kupiga kura na tuzo zimegawanywa katika makundi makuu matatu ambayo ni tuzo maalum za kitaifa, tuzo za vyombo vya habari na tuzo za kisekta,” ilisema taarifa hiyo.

Comments

Popular posts from this blog

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

SMZ yawaita vijana kushiriki kilimo