2.4trl/- kuing'arisha elimu 2025/26

NA SAIDA ISSA, DODOMA

WAZIRI ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeomba kuidhinishiwa shilingi trilioni 2.4 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli zake kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Katika kipindi hicho, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wadau wa elimu na umma kuhusu sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014, toleo la 2023 pamoja na utekelezaji wa mitaala iliyoboreshwa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, akiwasilisha makadirio ya bajeti ya wizara hiyo, alisema Serikali imepanga kutoa mafunzo kwa wathibiti ubora wa shule, walimu wa shule za msingi na sekondari, wakufunzi wa vyuo vya ualimu, maafisa elimu, wakufunzi wa vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi, pamoja na wahadhiri wa vyuo vya elimu ya juu.

Alieleza kuwa serikali itakamilisha mapitio ya Sheria ya Elimu Sura ya 353 ili iendane na matakwa ya Sera ya Elimu na Mafunzo 2014 (Toleo la 2023), sambamba na mapitio ya sheria nyingine za taasisi mbalimbali zinazohusika na elimu kama vile Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Bodi ya Huduma za Maktaba, Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Tume ya Vyuo Vikuu (TCU), na taasisi nyingine zinazotoa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi.

Aidha Prof. Mkenda alisema Serikali itakamilisha zana muhimu za utekelezaji wa sera, ikiwemo Mwongozo wa Upimaji na Tathmini katika Elimu, Mfumo wa Taifa wa Upimaji na Tathmini, na Mfumo wa Taifa wa Mitaala ili kuhakikisha utekelezaji wenye ufanisi wa sera hizo.

“Serikali itaandaa na kuhuisha miongozo mbalimbali inayohusu utoaji wa elimu na mafunzo, ikiwa ni pamoja na mwongozo wa kiunzi cha mahitaji ya walimu na usambazaji wao kwa lengo la kuimarisha usawa kulingana na mahitaji ya shule”, alieleza Prof. Mkenda.

Kadhalika alisema kuwa serikali pia itaandaa mwongozo wa kitaifa wa kuwaendeleza kitaalamu wakufunzi na wafanyakazi wasio wakufunzi katika vyuo vya elimu ya ufundi.

"Mwongozo wa ushirikiano baina ya viwanda na taasisi za elimu ya ufundi, Mwongozo wa Utambuzi wa Ujuzi katika Elimu ya Ufundi, Mwongozo wa kushughulikia masuala mtambuka katika taasisi 49 za elimu ya juu, Vilevile serikali itaandaa mwongozo wa uanzishaji wa kampuni na vituo vya ubunifu wa teknolojia (TICs) katika taasisi za elimu ya juu (umma na binafsi) na taasisi za utafiti wa maendeleo (RDIs), pamoja na kuhuisha miongozo ya udahili, upimaji, ithibati, elimu ya watu wazima, na elimu nje ya mfumo rasmi", alisema.

Kwa mara ya kwanza, Serikali itaanzisha programu ya Mama Samia 360 – DSP/AI+, itakayotoa ufadhili kwa wanafunzi waliofaulu kwa viwango vya juu katika masomo ya sayansi (kidato cha sita) kusomea shahada ya kwanza kwenye vyuo vikuu mahiri duniani katika fani za Data Science, Artificial Intelligence (AI), na Machine Learning (ML).

Katika eneo la sayansi na teknolojia ya nyuklia, Serikali itaendelea kutoa ufadhili kwa wanafunzi wenye ufaulu wa juu kwa ngazi ya shahada na shahada ya juu kupitia SAMIA Extended Scholarship.

Pia serikali itaanza utekelezaji wa SAMIA Innovation Fund yenye thamani ya Shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kutoa mikopo nafuu kwa wabunifu, ili kuwezesha ubunifu kubiasharishwa na kutoa ajira kwa Watanzania.

"Ili kuchochea tafiti bora, Serikali itaendelea kutoa tuzo ya Shilingi milioni 50 kwa tafiti zitakazochapishwa katika majarida ya kimataifa yenye hadhi ya juu, serikali itaendeleza elimu ya amali kwa kupanua shule 55 kuwa sekondari za amali, kuimarisha miundombinu ya vyuo vya ualimu wa amali (Mtwara Kawaida na Ufundi), na kuanzisha vyuo vipya vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi", alisema.

Serikali pia itajenga na kukarabati vyuo 54 vya maendeleo ya wananchi, kuanza awamu ya pili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Dodoma (ikiwa ni pamoja na mabweni, maktaba, karakana, nyumba za watumishi, na ukuta), na maktaba ya kisasa katika Chuo cha Ufundi Arusha.

Mradi mwingine utahusisha ujenzi wa mtambo wa nguvu za maji Kikuletwa na kupanua maabara ya udongo Arusha. Vilevile, Serikali itatekeleza Mradi wa TELMS II kwa ajili ya kuanzisha vituo vya ujasiriamali na ubunifu katika taasisi mbalimbali.

Serikali itaongeza idadi ya wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu kutoka wanafunzi 245,314 mwaka 2024/25 hadi 252,773 mwaka 2025/26. Vilevile, mikopo kwa wanafunzi 10,000 wa stashahada katika fani za sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati itaendelea kutolewa.

"Ufadhili kupitia SAMIA Scholarship utatolewa kwa wanafunzi 2,630 wenye ufaulu wa juu, ikiwa ni pamoja na wanafunzi 50 wa kike waliomaliza kidato cha sita,

Serikali pia itaendelea kuboresha ukusanyaji wa mikopo iliyoiva yenye thamani ya Shilingi bilioni 210.2 na kutambua wanufaika wapya 40,000,"alisema.

Prof. Mkenda alisema Serikali itakamilisha mapitio ya muundo wa COSTECH, kuboresha mifumo ya TEHAMA inayounganisha taasisi za elimu na utafiti, kufadhili tafiti 40 (19 kuhusu tabianchi na 21 viwanda), na kuendelea kugharamia vigoda vya utafiti katika taasisi za Nelson Mandela na SUA.

Serikali itaendelea kuandaa Dira ya Taifa ya Teknolojia 2050 itakayohusisha sekta mbalimbali ikiwemo elimu, lugha, biashara, afya, kilimo, haki za binadamu na TEHAMA kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Comments

Popular posts from this blog

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni

SMZ yawaita vijana kushiriki kilimo