Mbunge Ikupa ahimiza wenye ulemavu kulinda amani

NA SAIDA ISSA, DODOMA

MBUNGE wa Viti Maalum Stella Ikupa amewahimiza watu wenye ulemavu kuendelea kuenzi hali ya amani na utulivu vilivyopo nchini na kuwataka kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani.

Akizungumza wakati akifungua kongamano la watu wenye ulemavu lililoandaliwa na Ikupa Trust Fund alisema watu wenye ulemavu ni moja ya makundi ya Mwanzo yatakayopata shida kama machafuko yatatokea kwa sababu yoyote ile .

"Ninawaomba ndugu zangu,tunapoelekea katika uchaguzi mkuu, tuendelee kuiombea nchi yetu amani iendelee kudumu, tusikubali kuwa sehemu ya jambo lolote ambalo ni kinyume ,maana machafuko yakitokea nchini ,sisi walemavu ndio waathirka wa kwanza, tukifiatiwa na akina mama na watoto, tumuombe Mwenyezi Mungu uchaguzi uwe wa amani, tukatae wanahamasisha virugu”, alisema Ikupa.

Aidha Ikupa alitumia fursa hiyo kuipongeza serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa mambo mengi iliyifanya kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

"Serikali ya awamu ya sita imeendelea kufanya mambo makubwa kwa watanzania lakini yapo mambo maalum yanayowagusa watu wenye ulemavu ikiwemo ujenzi wa miundombinu katika majengo ya Serikali na yasiyo ya serikali kwa ajili ya watu wenye ulemavu”, alisema Mbunge huyo.

Katika hatua nyingine ameishukuru serikali na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kuweka utaratibu wa kuwapata wawakilishi wa watu wenye ulemavu Bungeni lakini pia kumpa fursa na kuhudumu kama Mbunge katika kipindi chake chote cha uongozi.

Kadhalika aliviomba vyama vyote kuweka utaratibu wa kuwapata wawakilishi wao watakaoingia Bungeni kupitia kundi la wenye ulemavu Ili kuongeza wigo wa watunga sera kupitia kundi hilo.

"Lakini na sisi tuzungumze huko kwenye vyama vyetu kwamba tunahitaji nafasi hizo tusikae kimya tukitegemea kuna mtu mwingine atatuzungumzia kile tunachohitaji”, alisema.

Hivyo aliwataka washiriki wa kongamano hilo, kwenda kuelimisha na wengine ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria kongamano hilo huku akihimiza viongozi wa vyama vya wenye ulemavu waendelee kuongeza wanachama Ili iwe rahisi kupata huduma maeneo mbalimbali ikiwemo serikalini.

Comments

Popular posts from this blog

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni

SMZ yawaita vijana kushiriki kilimo