Wafikieni watumishi wa ngazi za juu, viongozi waandamizi – Mhandisi Zena

NA MWANAJUMA SAID, IPA

KATIBU wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Mhandisi Zena Ahmed Said, amelitaka Chuo cha Utawala wa Umma Zanzibar (IPA) kuwafikia watumishi wa kada za juu na viongozi waandamizi ili kuongeza ufanisi katika usimamizi na utoaji wa huduma za umma.

Akizungumza wakati wa mahafali ya 18 ya chuo hicho huko Tunguu, alisema kuwa kwa muda mrefu IPA inatoa mafunzo ya muda mfupi yanayolenga zaidi watumishi wa kada za chini na kati, wakati kundi la viongozi wa ngazi za juu likibaki nyuma kupata mafunzo maalum yanayohitajika katika nafasi zao pekee.

“Kuna haja sasa kuelekeza nguvu za kuwafikia watumishi wa kada za juu na viongozi. Ni muhimu viongozi wa ngazi zote wafikiwe kulingana na mahitaji yao ya mafunzo na upatikanaji wao”, alisema Mhandisi Zena.

Alisema kuimarika kwa mafunzo hayo kutachochea maboresho ya mifumo ya uongozi, kuongeza uwajibikaji na kuleta matokeo chanya kwa wananchi katika taasisi za umma.

KATIBU wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Mhandisi Zena Ahmeid Said, akimkabidhi Sabia Salum Abdalla, cheti cha mwanafunzi bora wakatika mahafali ya 18 yaliyofanyika ukumbi wa Dk. Ali Mohammed Shein wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Tunguu Unguja.

Aidha, aliwahakikishia wahitimu na watendaji wa chuo kuwa Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Katibu Sheria Utumishi na Utawala Bora itatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha viongozi wanapatikana na kushiriki kikamilifu katika mafunzo yanayopangwa.

Akizungumzia eneo la utafiti na ushauri elekezi, Mhandisi Zena alisema ni lazima chuo kutoa kipaumbele, kwani ndicho chanzo cha maarifa ya kisayansi yanayowezesha Serikali kutambua na kutatua changamoto zinazolikabili taifa sasa na zijazo.

Kwa upande wa wahitimu, aliwakumbusha kuwa elimu wanayopata haina thamani endapo haitatekelezwa kwa vitendo katika maeneo ya kazi kwa kuwa mafunzo waliyoyapata ni msingi muhimu wa ujenzi wa uwezo wa kitaaluma kwa jamii na taifa.


KATIBU wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Mhandisi Zena Ahmeid Said, akikabidhi cheti kwa mfanyakazi bora wa IPA 2025, Khamis Mohammed Kheri wakati wa mahafali ya 18 ya chuo hicho ukumbi wa Dk. Ali Mohammed Shein wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Tunguu Unguja.

Akisoma risala, Mkuu wa Chuo cha IPA, Dk. Shaaban Mwinchum Suleiman, alisema chuo kinaendelea kupanua wigo wa huduma kwa kuboresha ubora wa elimu na mafunzo ya uongozi.

Alieleza kuwa chuo kimeanzisha kwa Shahada ya Uzamili ya Sayansi ya Uongozi wa Rasilimali Watu (MSc in HRM), programu ya mwaka mmoja na nusu iliyoandaliwa kukidhi mahitaji ya kuandaa wataalamu na viongozi wenye uwezo wa kusimamia watu, kupanga mifumo ya kiutendaji na kufanya maamuzi ya kimkakati.

“Tunataka wahitimu wetu wawe nguzo ya mabadiliko, wenye uwezo wa kufikiri kimkakati na kuunda mifumo imara ya uongozi,” alisema Dk. Mwinchum.

BAADHI ya Wakufunzi wa Chuo cha Utawala wa Umma (IPA) wakishiriki mahafali ya 18 ya chuo hicho yaliyofanyika katika ukumbi wa Dk. Ali Mohammed Shein wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Tunguu Unguja.

Aidha aliwasisitiza wahitimu kuzingatia maadili, bidii, na kuiona elimu kama safari endelevu inayohitaji kujifunza kila wakati ili kuendana na mabadiliko ya dunia ya sasa.

Nae Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, Mmanga Mjengo Mjawiri, alisema Baraza limeendelea kusisitiza umuhimu wa IPA kuongeza nguvu katika utoaji wa mafunzo mafupi, ambayo ni njia ya haraka ya kuongeza ujuzi wa watumishi na kuchochea ufanisi katika utumishi wa umma.

“Tumekuwa tukihimiza chuo kujikita kwenye mafunzo mafupi kwa kuwa ndiyo njia ya kuongeza ujuzi wa watumishi kwa haraka”, alisema.

SEHEMU ya Wahitimu wa Chuo cha Utawala wa Umma (IPA) wakiwa katika mahafali ya 18 ya chuo hicho ukumbi wa Dk. Ali Mohammed Shein wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Tunguu Unguja.

Nao baadhi ya wahitimu waliahidi kutekeleza nasaha walizopewa na viongozi, wakisema dhamira yao ni kuendelea kujiboresha kielimu na kitaaluma, kwa kuzingatia msemo kuwa elimu haina mwisho.

Katika mahafali hayo, jumla ya wahitimu 786 walitunukiwa vyeti katika ngazi mbali mbali, wakiwemo wanawake 474 na wanaume 312 katika programu za Astashahada, Stashahada na Shahada ya kwanza.


Comments

Popular posts from this blog

'Zanzibar Matibabu Card' yashinda tuzo ya WSIS

ZAMECO yakumbushia sheria mpya ya habari