NMB yaendelea kung'ara benki bora wateja binafsi
NA MWANDISHI WETU
BENKI ya NMB imeshinda tuzo ya benki kiongozi wa kuwahudumia wateja binafsi nchini kutokana na ubora wa huduma zake kukidhi mahitaji ya huduma za kifedha za umma wa walio wengi.
NMB ilitunukiwa tuzo hiyo kwenye hafla ya
tuzo za Global Banking and Finance (GBAF) zilizofanyika jijini London,
Uingereza zilizoanzishwa mwaka 2011 na jarida la Global Banking & Finance
Review lenye wasomaji zaidi ya milioni tatu ulimwenguni kote na ambalo shughuli
yake kubwa ni kuangazia matukio na maendeleo ya kifedha duniani kwa mwaka wa
pili mfululizo,.
Akizungumza kwenye hafla ya kuwazawadia
washindi wa tuzo za mwaka huu, Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB,
Filbert Mponzi, alisema ushindi wa benki hiyo ni kutambuliwa kwa dhamira yake
thabiti ya kuwawezesha wateja na kulihudumia kikamilifu taifa kwa ujumla.
“Tunawahudumia wateja binafsi wa aina
mbalimbali wakiwemo wakulima wadogo, watumishi wa umma, wafanyakazi wa sekta
binafsi na wajasiriamali wa kada zote kuanzia ile ya chini kabisa hadi wale wa
kati. Kwenye hilo hatuna mpinzani. Tupo kwa asilimia 100 katika wilaya zote
nchini,” Mponzi alisema.
Alieleza kuwa NMB inaongoza kwa kuwa na mtandao mpana wa usambazji huduma wenye matawi 227 ambayo asilimia 70 yake yapo maeneo ya vijijini, na zaidi ya NMB Wakala 15,000 pamoja na zaidi ya mashine za kutolea pesa 750.
“Dira na mkakati wetu wa sasa hivi na siku zijazo ni kuendelea kutumia maendeleo ya teknolojia za kidijitali kutuwezesha kulisukuma gurudumu la huduma jumuishi za kifedha kwa kutoa huduma zinazohimilika, rahisi na zinazofikiwa na wengi kwa wepesi,” alifafanua Mponzi.
Alisema mafanikio iliyonayo NMB yasingewezekana bila mchango na msaada wa Serikali na Benki Kuu ya Tanzania ambazo alisema zimesaidia benki hiyo kustawi na kushamili kwa kuweka mazingira wezeshi na rafiki ya biashara na shughuli za kibenki.
Mponzi pia alibainisha kuwa mipango na ushirikiano
wa benki hiyo na wadau wake wote umeiwezesha kuwa na matokeo chanya kwenye
jamii na kupelekea kuaminika sokoni. Hali hii imepelekea kukua kwa amana za
wateja kwa asilimia 24 hadi TZS trilioni 6.5 mwaka 2021.
Comments
Post a Comment