TANESCO yazindua programu kukuza usawa kijinsia
NA SAIDA ISSA, DODOMA
NA SAIDA ISSA, DODOMA
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO),
limezindua programu ya miaka minne ya mpango wa kuimarisha usawa wa jinsia wenye
lengo la kutatua changamoto za wanawake katika maeneo ya kazi ikiwemo ya
vitendo vya unyanyasaji.
Akizugumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo Naibu Waziri wa Nishati, Stephen Byabato, alisema mradi huo unalenga kutengeneza sera za shirika na kujenga uwezo kuhusu masuala ya unyanyasaji wa kijinsia.
Alisema mradi huo, utasaidia kuwepo kwa taarifa sahihi za unyanyasaji wa kijinsia katika shirika, kuruhusu fursa ya ukuzaji taaluma kwa wafanyakazi wanawake na kuongeza mafunzo kwa vitendo kwa wafanyakazi wanawake waliopo kazini.
Alieleza kuwa mradi huu unatekelezwa na TANESCO lengo ni kuhakikisha watumishi wanaofanya kazi katika taasisi hiyo wanapata haki sawa, lengo ni kuhakikisha nafasi zinazojitokeza zinahusisha jinsia zote bila ubaguzi na kujenga usawa.
"Katika mradi huo tumekubaliana kuunda kitengo maalumu ambacho kitakuwa na bajeti na kujengewa uwezo kuhusu masuala ya jinsia ili mtu anapopata changamoto awe na sehemu ya kwenda kusema na kupata msaada”, alieleza Byabato.
Aidha aliongeza kuwa kuwepo kwa kitengo hicho ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020/2025 ambayo imeeleza serikali mambo mbali mbali ikiwemo uanzishwaji wa madawati ya jinsia.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi ya TANESCO, Balozi Mwanaidi Maajar (pichani) alisema maendeleo hayawezi kuwepo kama hakutakuwa na usawa wa kijinsia.
Alisema wanawake wamekuwa hawapewi kipaumbele katika nafasi kubwa za uongozi na ukizingatia sensa ya watu na makazi ya mwaka jana inaonyesha idadi ya wanawake ni wengi kuliko wanaume.
“Tunataka wanawake wa TANESCO wawe na haki na wajibu sawa na wanaume kusiwepo na vitendo vya vitisho akashindwa kufanya maamuzi mbalimbali,pia katika meza ya maamuzi na wanawake nao washirikishwe ili kujenga usawa mahali pa kazi,” alieleza Balozi Maajar.
Awali akitoa salamu za wafanyakazi wa TANESCO, Mkurugenzi Mtendaji wa Maharage Chande, alisema mradi huo ni ajenda ya kudumu katika taasisi hiyo.
Alisema TANESCO wamebahatika kupatia mradi wa kusafirisha umeme mkubwa kutoka na Tanzania kwenda Zambia (TAZA) unaofadhiliwa na serikali na wadau wengine hivyo swa la jinsia ni lazima lizingatiwe.
“Katika
mradi huu kuna kiapo cha kuangalia masuala ya usawa wa kijinsia, na lengo
la kuzindua mradi huu ni kuongeza chachu ya uwepo wa usawa katika masuala yote
katika taasisi yetu,” alisema Chande.
Comments
Post a Comment