Majaliwa awawashia moto watendaji wanaodaiwa 'kukwapua' mamilioni
NA MWANDISHI WETU, DODOMA
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa (pichani) amewasimamisha kazi mkaguzi Mkuu, Mkaguzi Msaidizi na baadhi ya
watendaji wa wizara ya Fedha na Mipango ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za
matumizi mabaya ya fedha za umma zinazowakabili.
Alichukua hatua hiyo katika kikao kazi na waziri wa Fedha na Mipango, Kaibu Mkuu, Manaibu Katibu Wakuu na Watendaji Waandamizi wa Wizara hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma.
Mbali ya hatua hiyo, Majaliwa
amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa
(TAKUKURU), Kamishna wa Polisi, CP Salum Rashid Hamdun kufanya uchunguzi kuhusu
tuhuma hizo na ikithibitika kwamba tuhuma si za kweli wahusika watarejeshwa
kazini.
Majaliwa alizitaja baadhi ya
tuhuma hizo kuwa ni malipo yaliyofanyika Machi 31, mwaka
huu kupitia vocha 30 ya shilingi milioni 251 yakielezwa kuwa ni
malipo maalum bila kutaja kazi hiyo maalum ni kazi gani na nani aliifanya hiyo
kazi.
Alisema siku hiyo
hiyo ya Machi 31 pia zililipwa shilingi milioni 198.8 kwa
madai kuwa ni posho ya honoraria.
Majaliwa alisema
Aprili 8 mwaka huu watumishi 27 wa wizara hiyo walilipwa shilingi
milioni 44.5 zikiwa ni posho ya kazi maalum ya wiki nne. Pia Aprili 13
mwaka huu zililipwa shilingi milioni 155.2 kwa watumishi 68 ikiwa ni posho ya
kazi maalum ya wiki tatu.
Aidha, Aprili 30 mwaka huu
zililipwa shilingi milioni 43.9 kwa ajili ya kuandaa mpango wa
kuhifadhi mazingira na siku hiyo hiyo zililipwa shilingi milioni 14.4 kwa ajili
ya siku ya wanawake. Fedha nyingine shilingi milioni 43 zililipwa siku hiyo na
kufanya jumla ya malipo yaliyolipwa siku hiyo kuwa shilingi milioni 101.8.
Alisema kuwa, Mei mosi mwaka
huu zililipwa shilingi shilingi milioni 184.1 na mchana zililipwa shilingi milioni
264 zikiwa ni malipo ya kazi maalum. "Sisi tulikuwa Mwanza tunasherehekea
siku ya wafanyakazi duniani nyinyi hapa ndani mnalipana posho”,alisema.
Aliongeza kuwa Mei 3 mwaka
huu zililipwa shilingi milioni 146.5 kwa watumishi 125 zikiwa ni malipo
ya kuandaa mpango kazi wa manunuzi kazi ambayo ni sehemu ya majukumu
yao ya kila siku, ambapo tarehe hiyo hiyo zililipwa shilingi milioni
171.2 kwa ajili ya kuandaa nyaraka za Bunge.
Majaliwa alisema shilingi
milioni 155 zililipwa kwa baadhi ya watumishi zikiwa ni posho ya kuandaa
miongozo ya kazi. " Yaani hii kazi ya ukaguzi imelipwa kwenye maeneo manne, huu ni utaratibu wa wapi?
Mnazidi kutupunguzia imani, na sijaongea eneo la kuhamisha mafungu
na utaratibu wa kuhamisha fedha kisha mnakwenda kuzichukuwa huko
mlikozihamishia."
Majaliwa aliwataka watendaji
wa wizara hiyo kujenga uaminifu kwa wanaokusanya mapato kwa kufanya kazi kwa
uaminifu na alitahadharisha kuwa watakaoendekea kucheza na pesa za umma hatua
kali zitachukuliwa dhidi yao.
Aidha, waziri mkuu
aliwapongeza watendaji wengine wa wizara hiyo ambao wameendelea kufanya kazi
kwa weledi “na nimesema hapa si wote wenzenu wachache wanatumia vibaya nafasi
zao kutuchafua wizara ya fedha”.
Comments
Post a Comment