Othman akutana na balozi wa Uingereza, Mwakilishi UNICEF
NA MWANDISHI WETUMAKAMU wa Kwanza wa Rais wa
Zanzibar, Othman Masoud Othman, amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,
imekubali kufanya kazi na Serikali ya Uingereza katika mapambano dhidi ya
uhalifu wa kidunia, likiwemo suala la dawa za kulevya kwa lengo la kuendelea
kuilinda Zanzibar na watu wake.
Othman amesema hayo alipofanya
mazungumzo na Msaidizi Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Rick Shearn, wakati
Balozi huyo alipofika kwa ajili ya kujitambulisha kwa Makamu wa Kwanza wa Rais
wa Zanzibar ofisini kwake Migombani, mjini Unguja.
Balozi Shearn ameonesha azma ya serikali
ya Uingereza kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwenye
masuala kadhaa, likiwemo hilo la kupambana na uhalifu unaovuuka mipaka ya
mataifa.
Alisema bado kuna mambo yanaendelea
kuiumiza dunia hasa suala la madawa ya kulevya na ufichwaji wa fedha za
kihalifu.
“Serikali imekubaliana kupitia
vyombo mbalimbali vinavyohusika na usimamizi wa sheria, uchunguzi, usimamizi wa
kodi pamoja na vile vinavyosimamia maeneo makuu ya kuingia Zanzibar, kufanya
kazi pamoja na Uingereza kwa lengo la kudhibiti uhalifu huu wa kidunia,“
alisema Othman.
Aidha othman, aliongeza kwamba
Balozi Shearn ameahidi kutoa ushirikiano katika kuvijengea uwezo vyombo hivyo
pamoja na kutanua wigo wa ushirikiano na vyombo vya kimataifa.
Sambamba na hilo, Uingereza
imeahidi pia kuongeza nguvu ili kuboresha uwepo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa
Zanzibar.
Wakati huo huo, Othman alikutana na
muwakilishi wa UNICEF nchini Tanzania, Shalin Bahugana, ambaye ameihakikishia
Serikali ya Zanzibar mashirikiano ili kuhakikisha kuwa Zanzibar inaendelea kuwa
vyema katika masuala mbali mbali ya kiafya na maisha kwa vijana wake.
Mwakilishi huyo alisema wamejipanga
kuja na mkakati maalum wa kuwasaidia vijana kutokana na changamoto za kimaisha
na za kiuchumi kwa kutoa taaluma juu ya kujenga maisha yao.
“Sisi katika UNICEF tumeandaa
mpango mkubwa kuhusiana na utoaji wa taaluma juu ya lishe bora, jambo ambalo
limekuwa tatizo kwa wananchi walio wengi kujisimamia katika suala zima la
ulaji, na hivyo kupelekea kukosa jamii iliyo bora,“ alisema Bahugana.
Kwa upande wake, Makamu wa Kwanza
wa Rais wa Zanzibar alimuhakikishia mwakilishi huyo wa UNICEF kuwa serikali itaendelea
kuungana nao pamoja katika kuhakikisha jamii ya Zanzibar inakuwa na ustawi
mzuri, hasa katika suala la afya.
Comments
Post a Comment