Serikali itawapa kipaumbele wajasiriamali wanawake
NA MWANDISHI MAALUM, OMKR
Mke wa Makamu wa
Kwanza Wa Rais wa Zanzibar, Zuhra Kassim
Ali, (wa pili kushoto), amesema serikali imejipanga kuwahudumia wananchi wote na hasa
wajasiriamali wanawake, kwa kutatua kero zao kwa haraka ili kuendelea kuweka
mazingira bora ya kutekeleza shughuli zao za kiuchumi.
Zuhra ameyasema
hayo katika mahafali ya mafunzo ya ujasiriamali kwa wanawake yaliyoendeshwa kwa
njia ya mtandao yaliyofanyika katika ukumbi wa wakfu ya Wangazija Forodhani Jitini,
ambayo yalioandaliwa na Taasisi ya Wanawake Wajasiriamali (AWE) kwa
ufadhili wa Serikali ya Marekani.
"Serikali
inaendelea kusimamia jambo hili kwa karibu ili kuhakikisha wajasiriamali wote
wanapata mazingira mazuri kwa ajili ya kufanya shughuli zao za ujasiriamali,"
alieleza Zuhra.
Hivyo Zuhra
aliwataka Wanawake hao kuitumia vyema fursa na elimu waliyoipata katika mafunzo
hayo ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiuchumi.
"Nawaomba
sana wahitimu, kufanya kazi kwa mashirikiano baada ya kupata mafunzo haya
na kuwaelimisha wajasiriamali wengine waliokosa fursa hii ili kusaidia
kuboresha biashara zao, kupambana na changamoto ya ajira pamoja na kuinua
uchumi wa taifa kwa ujumla," alinasihi Mke wa Makamu wa Kwanza wa Rais.
Kwa upande wake Muwakilishi
wa Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Amy Hart Vrampas, alisema lengo la mradi
huo ni kuona wanawake wanakuwa chanzo kikubwa cha maendeleo kwa kuwapatia ujuzi
wa kujiwezesha kujipatia kipato cha kila siku.
Akisoma risala fupi
iliyoandaliwa na wanafunzi waliomaliza mafunzo hayo Ndg. Mwanaidi Said,
wameiomba Serikali kuunga mkono jitihada hizo ili waweze kunyanyuka kiuchumi
pamoja na kuwapatia fursa mbali mbali za kimaendeleo.
Katika hafla hiyo
wanafunzi 17 wametunikiwa vyeti kwa kuhitimu mafunzo hayo yalioanza mwezi wa
kwanza hadi wa sita mwaka 2021 ikiwa ni mara ya kwanza kwa taasisi ya AWE kutoa
mafunzo hayo hapa Zanzibar.
Comments
Post a Comment