TMA kujenga vituo saba vya rada
NA SAIDA ISSA, DODOMA
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema katika mwaka wa fedha 2022/2023 imejipanga kujenga vituo vya rada saba pamoja na vifaa vitakavyosaidia kuangaza nchi masaa 24.
Akizungumza na waandishi wa
habari jijini Dodoma, Mkurugenzi Huduma
za Utabiri wa TMA, Dk. Hamza Kabelwa, kuhusu majukumu ya mamlaka hiyo na
mwelekeo wa utekelezaji kwa Mwaka wa fedha 2022/23 amesema kuwa licha ya
kuanzisha miradi hiyo, wataalamu wamepatiwa mafunzo kwa ajili ya kuendesha rada hizo.
“Mafunzo kwa wahandisi na waendesha
mitambo kuhusu kuzihudumia na kuzitumia rada hizo yalifanyika kiwandani nchini Marekani.
Aidha utengenezaji wa rada mbili za mwisho zitakazofungwa KIA (uwanja wa ndege
wa kimataifa Kilimanjaro) na Dodoma ulifikia asilimia 45 ambapo mamlaka ilifungua
barua ya dhamana kwa ajili ya malipo ya asilimia 80 ya utengenezaji wa Rada
hizo,” amesema Dk. Kabelwa.
Alifafanua kwamba kukamilika kwa
rada hizi kutakamilisha mtandao wa rada nchini kufikia saba rada ambazo zina uwezo
wa kuona zaidi ya kilomita za mkato 450 huku zikizunguka na kuona matone madogo
sana ya mvua katika hali ya uhalisia ndani ya kilometa 250.
Akizungumzia mikakati ya mamlaka
hiyo Dk. Kabelwa amesema mamalaka hiyo imejipanga kupanua wigo wa utoaji wa
elimu kwa wananchi na wadau wengine juu ya umuhimu wa huduma za hali ya hewa na
kuendelea na utekelezaji wa Sheria Na.2 ya mwaka 2019 na Kanuni zake.
“Tumedhamiria kuimarisha uangazi wa
hali ya hewa katika bahari na maziwa makuu ili kuimarisha usalama wa abiria wa
kwenye maji, shughuli za uvuvi pamoja na kusaidia shughuli mbalimbali zikiwemo
upakuaji wa mizigo bandarini na uvunaji wa gesi asilia,” amefafanua.
Ameongeza kuwa; “Tumejipanga kufanya ufuatiliaji kwa wakandarasi wanaotengeneza Rada na vifaa vya hali ya hewa ili vikamilike na kuwasili nchini na kuhakikisha wadau wote wenye vifaa vya hali ya hewa nchini wanavifunga vifaa hivyo kwa kuzingatia Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Na. 2 ya mwaka 2019 na Kanuni zake”.
Aidha amesema mpango mwingine ni kuongeza
vyanzo vya mapato kwa lengo la kuboresha huduma za hali ya hewa, kuendelea
kuboresha miundombinu ya Chuo cha Taifa cha Hali ya Hewa na kuandaa miradi yenye
lengo la kupata rasilimali kutoka kwa washirika wa maendeleo ndani na nje ya
nchi ili kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.
Ameongeza kuwa TMA inaendelea na juhudi za kuongeza mapato
kwa kuwafikia wadau wake na kuwaeleza juu ya umuhimu wa kutumia huduma za hali
ya hewa ambapo amesema Jitihada
zimepelekea mapato ya Mamlaka kuongezeka kwa asilimia 53% katika mwaka
wa fedha 2021/22.
Hata hivyo Dk. Kabelwa amesema mamlaka
hiyo inaendelea kutoa elimu kwa jamii juu ya tafsiri ya taarifa zinazotolewa na
watu mbali mbali ambazo hazina usahihi juu ya masuala ya hali hewa na vipindi
vya mvua hapa nchini.
Comments
Post a Comment