ZMBF, Afya Checkers kuimarisha kampeni ‘Afya Bora, Maisha Bora’
NA MWANDISHI WETU
TAASISI
ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF) imeingia makubaliano ya ushirikiano
na Afya Checkers ya jijini Dar es salam kwa ajili ya kutoa huduma za afya kupitia
kampeni ya ‘Afya Bora, Maisha Bora’ inayoendeshwa na taasisi hiyo kupitia
matembezi ya ‘Mariam Mwinyi Walkathon’.
Matembezi hayo
ambayo ni mwendelezo wa kampeni ya mama Mariam aliyokua akiifanya kupitia
matembezi ya kila mwisho wa mwezi, yanatarajiwa kufanyika Septemba 30, mwaka
huu kwa kutanguliwa na kambi ya matibabu itakayofanyika Septemba 28 na 29.
Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini makubaliano hayo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa ZMBF, Fatma Fungo, alieleza hatua hiyo inalenga kuyaimarisha matembezi hayo na kutoa fursa kwa wananchi kupata huduma za afya.
Aidha Fungo alisema
katika awamu ya kwanza ya kampeni hiyo, matembezi hayo yalifanyika katika
wilaya zote za Zanzibar kwa kushirikisha wadau mbali mbali kwa lengo la
kuimarisha afya zao.
MAOFISA Watendaji Wakuu wa Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), Fatma Fungo (kulia) na Afya Checkers, Dk. Ramona Malikusema, wakibadilisha hati za makubaliano ya ushirikiano ya utekelezaji wa kampeni ya ‘Afya Bora Maisha Bora’ baada kutiaana saini wa makubaliano hayo katika ofisi za ZMBF, Migombani Zanzibar.
“Mara ya mwisho matembezi hayo yalifanyika kisiwani Pemba ambapo watu zaidi ya 3,000 walijitokeza kumuunga mkono mama Mariam Mwinyi (Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapiduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi) katika matembezi na mazoezi ya viungo ili kujenga miili yao”, alieleza Fungo.
Akizungumzia
marathoni hiyo, alieleza itafanyika kila baada ya miezi mitatu na kwa lengo la
kuyaimarisha yatajumuisha utoaji wa huduma za uchunguzi, upimaji na matibabu wa
maradhi mbali mbali zitakazotolewa na wataalamu wa afya kutoka ndani na nje ya
Zanzibar.
Aidha aliishukuru
‘Afya Checkers’ kwa uamuzi wa kushirikiana na taasisi yake jambo alilodai
litaongeza kasi ya kampeni hiyo iliyoasisiwa na mama Mariam ambaye pia ni
Mwenyekiti wa Bodi na Msarifu wa ZMBF.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa ‘Afya Checkers’, Dk. Isaac Maro (kulia), alieleza kuwa watatumi uzoefu walionao kufanikisha kampeni hiyo ili kutoa fursa kwa wananchi kupata huduma za afya na matibabu kwa urahisi.
Alisema taasisi
hiyo toka mwaka 2008/2009 imekua ikijihusisha na masuala ya utoaji wa elimu ya
afya na huduma za matibabu kupitia vyombo vya habari na kambi za matibabu kwa
kushirikiana na wadau kutoka serikalini na sekta binafsi.
“Muda wote huo
tumekua tukitoa hudua za afya na kuimarisha uelewa wa jamii kuhusu masuala ya
afya kupitia kambi maalum zinazojukmuisha madaktari na wataalamu wa afya kutoka
hospitali mbali mbali nchini”, alieleza Dk. Maro.
Alitaja miongoni
mwa huduma zinazotolewa na taasisi hiyo ni pamoja na uchunguzi wa maradi ya
kuambukiaza na yasiyo ya kuambukiza uakiwemo ya UVIKO 19 na huduma za
utengamano kwa watoto wenye ulemavu kupitia skuli.
“Pia kupitia kampeni mbali mbali tunafanya tafiti ambazo huwasaidia wadau wakiwemo watunga sera kufanya maamuzi juu ya aina ya huduma za kupeleka kwa jamii”, alieleza Dk. Maro.
Aidha alipongeza ZMBF kwa juhudi inazochukua kuimarisha jamii kupitia kampeni na programu mbali mbali hususani za afya jambo linaloongeza thamani ya taasisi hiyo mbele ya jamii.
Akizungumza kwa
niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya ZMBF, Nassir Ahmed Haji, ambaye ni Mjumbe wa
Bodi, alipongeza hatua hiyo na kuahidi kwamba bodi itatoa kila aina ya
ushirikiano kufanikisha utekelezaji wake.
Hivyo aliwataka
wadau wengine kuendelea kuunga mkono kampeni hiyo kwa kuwa ina faida kwa jamii
ikiwa ni miongoni mwa malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.
Comments
Post a Comment