Zaipuna awapa msukumo vijana kuikabili changamoto za karne ya 21
NA MWANDISHI WETU
AFISA Mtendaji Mkuu
wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna, amewashauri vijana nchini kunoa ujuzi wao wa karne
ya 21 ili kufanikiwa katika soko la kisasa la ajira lenye ushindani.
“Mkiwa na ujuzi huu, nina hakika kabisa kwamba mtafaulu
katika shughuli zenu za maisha iwe mnataka kuajiriwa au kujiajiri. Mtawavutia
waajiri na wawekezaji na kwa moyo wa kuendelea kujifunza, mtaimarika siku hadi
siku na kujiongezea thamani,” Zaipuna alisema.
Aliongeza, “Kwa miaka mingi, nimekuwa sehemu ya Shule za Feza
na ninathamini sana msisitizo ambao shule inaweka katika elimu ya maisha na
maendeleo, ushirikiano na jamii na ukuzaji wa stadi za uongozi, sifa ambazo
naamini zitakuwa na athiri chanya kwa watoto wetu kwa miaka mingi ijayo”, alisema.
Aidha Zaipuna alibainisha kuwa maisha ni safari na kuwataka
vijana hao kufanya kazi kwa bidii na kuongeza kuwa wanaweza kufikia chochote
wanachokusudia endapo wataendelea kuwa na nidhamu.
“Nilianza safari yangu takriban miongo mitano iliyopita.
Miaka 32 iliyopita, nilihitimu kidato cha nne katika Skuli Sekondari Kilakala,
Morogoro. Siku hii imenifanya kutafakari maisha yangu yote tangu nilipohitimu mwaka
1991”, alisema.
Hivyo aliwataka wanafunzi hao kujiamini, kufuata nafsi zao
na kamwe wasipoteze maadili na kanuni walizopandikizwa wakiwa shuleni.
Alibainisha kuwa baadhi ya vitu ambavyo vimesaidia kupanda
daraja la mafanikio ni pamoja na nidhamu, bidii, uadilifu, ubora katika kila
kazi iwe kubwa au ndogo na kuendelea kujifunza mambo mbalimbali.
“Licha ya vikwazo
ambavyo mmekumbana navyo mkiwa hapa, mmeibuka kuwa nyota zinazongaa. Katika
miaka yenu yote katika Shule za Feza, mmeonyesha dhamira isiyoyumba kwa
kuendela kufanya vyema. Mafanikio haya ni uthibitisho wa bidii zenu",
alisema.
Aliwashauri wahitimu hao kuchangamkia fursa zinazowajia huku
akiongeza kuwa mafanikio hayapimwi kwa alama au sifa tu, bali pia kwa matokeo
yanayopatikana katika maisha ya wengine.
Awali, Naibu Mkurugenzi wa Shule za Feza, Ali Nungu, aliwataka
wahitimu kuendeleza miiko ya shule hiyo ilikuleta mabadiliko katika njia
watakayochagua.
Aliwapongeza walimu wa shule hiyo, wafanyakazi wengine na
wazazi ambao walichukua jukumu kubwa katika safari ya wahatimu hao na kuwataka
wahitimu kuamini katika uwezo wao.
Alionyesha imani kwamba kwa tabia zao nzuri, uwezo bora wa
kitaaluma na ustahimilivu, watakuwa wakakamavu na wenye shauku katika kutimiza
ndoto zao.
Comments
Post a Comment