Absa Tanzania yahamasisha wajasiriamali kutumia huduma za kifedha
NA MWANDISHI WETU
BENKI ya Absa Tanzania imeendelea kuhamasisha wanawake wajasiriamali kutumia huduma rasmi za kifedha ili kuimarisha biashara zao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Hatua hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za benki hiyo katika kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia huduma zinazolenga kuongeza ujuzi wa usimamizi wa fedha, upatikanaji wa mitaji na matumizi ya teknolojia katika biashara.
Akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani jijini Dar es Salaam, ambayo Absa ilikuwa miongoni mwa wadau waliodhamini, Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa benki hiyo, Victor Nchimbi, alisema benki hiyo inatambua mchango mkubwa wa wajasiriamali katika kukuza uchumi.
MKUU wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Victor Nchimbi, akizungumza na wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambapo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini tukio hilo, jijini Dar es salaam hivi karibuni.
Alisema kupitia akaunti maalumu ya SHE, benki hiyo imeweka huduma zinazolenga kuwawezesha wanawake wajasiriamali kuendesha biashara zao kwa urahisi na ufanisi zaidi.
Alieleza kuwa akaunti hiyo haina makato ya kila mwezi ya uendeshaji, ina ada nafuu za miamala na inawawezesha watumiaji kufanya miamala kwa fedha za Tanzania pamoja na fedha za kigeni.
"Tunatambua mchango wa wajasiriamali Tanzania, hususan wanawake, ndiyo maana tumeendelea kuweka huduma mbalimbali ikiwemo mikopo yenye gharama nafuu, huduma za kidigitali na akaunti ya SHE inayolenga kuwawezesha wanawake kiuchumi," alisema Nchimbi.
Kwa upande wake, mmoja wa wajasiriamali anayejishughulisha na biashara ya vipodozi, Maua Jumanne, alisema changamoto kubwa inayowakabili wanawake wengi ni ukosefu wa elimu ya fedha, mitaji na maarifa ya kuendesha biashara kwa ufanisi.
Alisema hatua hiyo itasaidia kupunguza utegemezi wa baadhi ya wajasiriamali kwa mikopo isiyo rasmi yenye gharama kubwa na kuwawezesha kukuza biashara zao kwa mazingira salama.
Siku hiyo pia hutumika kuhamasisha mazingira bora ya biashara, upatikanaji wa mitaji, elimu ya ujasiriamali na sera zinazowawezesha wajasiriamali wadogo na wakubwa kufikia malengo yao.
BAADHI ya Wawezeshaji na Wajasiriamali walioshiriki Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukamilika kwa maadhimisho yaliyofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni ambapo benki ya Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini tukio hilo.





Comments
Post a Comment